Watoto tisa wa familia moja waungua moto kwenye nyumba walimokuwa wamelala, Musoma mjini nchini Tanzania.
Moto huo ulizuka usiku wa kuamkia Novemba 5, 2022 na kuunguza watoto hao tisa wa familia moja ambapo mmoja alifariki dunia wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Mkoa wa Mara na wengine wanane kujeruhiwa.

Watatu hali zao ni mbaya ambapo wamepelekwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando jijini Mwanza kwa matibabu zaidi.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na uokoaji mkoani Mara,Agostino Magere amesema tukio kuwa wakikamilisha uchunguzi wao wa chanzo cha tukio hilo watatoa taarifa kamili.
“Ni kweli tukio limetokea, mtoto mmoja amefariki na wengine watatu hali zao ni mbaya, tayari tumeanza uchunguzi tutatoa taarifa kamili baada ya kukamilisha uchunguzi wetu ” amesema Magere kwa njia ya simu na jarida la Mwananchi Tz.
Kulingana na baba mzazi wa watoto hao, Emmanuel Magiri amesema kuwa tukio hilo lililotokea baada ya umeme kukatika ndipo watoto hao waliokuwa wamelala pamoja kwenye chumba kimoja kuamua kuwasha mshumaa kwaajili ya kupata mwanga.
“Baada ya kuwasha mshumaa walipitiwa na usinguzi ndipo godoro walilokuwa wamelalia likashika moto na kusambaa chumba kizima” amesema
Magiri amesema kuwa akiwa amelala kwenye nyumba ya pili alisikia kelele za watoto kuomba msaada na alipotoka nje alikuta tayari chumba cha watoto kimeshika moto.
Amesema baada ya kuona chumba hicho kimeshika moto, alisaidiana na majirani kuwaokoa kutoka kwenye moto na kuwapeleka hospitali.
Daktari aliyewapokea watoto hao katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara, Dk Charles Paschal amesema kuwa baada ya watoto hao kupokelewa walipewa huduma ya kwanza lakini mmoja alifariki dunia akiwa anaendelea na matibabu hospitalini hapo.