Kamati ya kuteua mgombea mwenza wa muungano wa Azimio watapendekeza majina ya wanasiasa watatu bora zaidi kwa nafasi hiyo mnamo Alhamisi, Mei 12.
Mwenyekiti wa kamati hiyo ya watu saba Noah Wekesa ambaye ni waziri wa zamani alisema kwa sasa wanashughulikia matokeo ya mahojiano hayo na watakuwa na ripoti kamili siku ya Alhamisi Mei 12.
Wanasiasa kumi walihojiwa na kamati hiyo kinyume na 11 waliotarajiwa baada ya mwenyekiti wa chama cha KANU Gideon Moi kujiondoa kwa misingi kuwa jina lake liliwasilishwa bila idhini yake.
Waliohojiwa ni kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, mwenzake wa Narc Kenya Martha Karua, aliyekuwa Mbunge wa Gatanga Peter Kenneth, Waziri wa Kilimo Peter Munya, aliyekuwa Mbunge wa Emgwen Stephen Tarus, kiongozi wa Narc Charity Ngilu,Gavana wa Mombasa Hassan Joho,Gavana wa Nakuru Lee Kinyanjui,Gavana wa Kakamega Wycliffe Oparanya na Mbunge wa Murang’a Sabina Chege.